Tag

mbinguni


Browsing

Mwandishi: Mtoto Wa Katama

Fujo ziliendelea mle ndani, kweli mapambano yalikuwa yamechacha vyombo vilisikika vikianguka. Watu nao nje hamu na hamumu ziliwazidi kila mayoye yalipozidi. Waliamua wasingeweza kukosa uhondo wote huo, maana milango na madirisha yalikuwa yamefungwa yote na hawakupata kuona lolote. Jagina moja likatokea ili ‘kutafuta suluhu’ na kusukuma watu nyuma, akaanza kuonesha madoido kwa kukaza misuli yake ya mikononi. Watu walimshangilia na kumtia mori, akajawa na ushujaa akaja mbio kwa fujo, na kupita na mlango wa nje kwa bega lake. Naye kweli alikuwa na nguvuze, ule mlango kuuvunja kwa kishindo kimoja ni jambo la kupewa kongole kwa kazi nzuri aliyoifanya. Naye ‘ushujaa’ ule ulikuja na gharama alianguka kwa kishindo ukumbini na kujipiga na meza. Maskini ya Mungu! Alilia kama kitoto kidogo, bega lilikuwa khalas! tayari lilikuwa limevunjika.

Watu wakaanza kumiminika kuingia mle ndani, hata hawakudiriki kumpa usaidizi wa kwanza ‘shujaa’ wao aliyewavunjia mlango. Walimuacha akigaragara chini na kumruka bila hata ya kumjali na lolote. Punde si punde kila mtu alionekana akikimbilia kutoka nje. Mlango ukageuka ‘mdogo’ watu waliparamiana na kusukumana ili wapate nafasi ya kuregea walipotokea. Vilio viliskika tu sana kwa wingi,na wale waliokuwa nje walishindwa kwa nini wenzi wao wanaregea tena kwa kishindo. “Anakuja tayari kashamaliza huko ndani!”

Kila mtu roho mkononi, kwa mda wa sekunde chache kimya kilitalawa sehemu yote, kama vile wakati ulikuwa umesimamishwa na hakuna kilichosonga. Mara ghafla! Bwanamkubwa Khamisi alichopoka na panga likiwa mkononi, nguo zake zilikuwa zimelowa damu ajabu. Lo! Lile panga lilivyokuwa likitiririka ngeu…..Mmmmhh! kweli asiyekuwa na macho haambiwi tazama. Kwani kuna la zaidi l kuambiwa! Kila mtu tayari alipata picha kamili ya tukio lilojiri. Na kilichobaki  ilikuwa mguu niponye, waliokuwa mbele ya tukio walianza kutawanyika na kusambaratika wakielekea kila upande. Walimpa Khamisi njia, utadhani rais keshaingia mjini, hakuna aliyedhubutu kujifanya shujaa….ili iweje? Kwa kasi ile aliyokuwa akikimbia nayo Khamisi, hakuna ambaye angeweza kumkamata au kudhubutu kumzuia.

Khamisi alitokomea baada ya kupiga vichochoro kadha na kuacha vilio nyuma! Mwili wa ami yake Khamisi alikuwa amelala kifudifudi katika ‘kidimbwi’ cha damu, mwili wake alikuwa amechanjwa chanjwa kwa panga. Teyari mtu keshaenda jongomeo, mwenye roho nyepesi asingeweza kumudu kuangalia mwili ule. Unyama ulioje ule, kila aliyetoka mle ndani alikuwa ameshika kichwa na kuonyesha hali ya kutamaushwa na tukio lile. Mamake Khamisi aligaragara chinina kupiga mayowe, alitoa leso yake na kuanza kuichanachana kwa uchungu. Jirani zake walijaribu kumuauni, lakini wapi waliambulia patupu. Hakuamini katu kisa alichokifanya mwanawe…”Laana gani umeniachia babake Khamisi? Mbona mimi tu” aliomboleza mamake Khamisi kwa fujo, huku machozi yakimdondoka kwa wingi. “ Mama utakufuru Mungu sasa! Ebu! Jitande kwanza na umuogope Mungu” mmoja wa jirani zake alijaribu kumsemesha apunguze maombolezo yake asije akavuka mipaka. Kwa kweli ya Mungu ni mengi, hakuna yeyote aliyedhania matukio kama haya yangetokea, siku ilianza kwa uzuri na utulivu, na jinsi ilivyopinduka kwa ghafla! Kwa muda wote ule watu wakiponda jinsi ya kufanya, kila mtu alijiuliza “ Je Khamisi yuko wapi?……………..

Mwandishi: Mtoto wa Katama

 

“Kesha pagawa! Wallahi ameshakuwa chizi, lakini ole wake akili zikimarudia atatulipa biashara zetu sote” nyuma sauti ziliskika zikilaani kwa hasira. Lakini Khamisi hakuwa na shida nao, ni umbea wao tu uliowachongea, yaani hivi ukiona mtu akija mbio na panga na nyinyi eti mnaamua kukimbia….eti ehh?  Swali hilo. Yaani mnakurupuka tu ovyoo! Na kujijeruhi na kusababisha hasara biashara zenu…kwani hamjawahi kuona wamasaai wakizunguka na sime zao viunoni? Na wala hamjawahi kukimbia, bivi leo mnamuonea ajabu Khamisi. Khamisi naye yeye alikuwa anakimbizwa na ajenda zake, mbio zote hizo alikuwa akielekea kwa ami zake.

 

“Mamake Zeituni hivi umemuona Khamisi!” mamake Khamisi aliuliza kwa mshangao, baada kuona mlango wa chumbani mwake uko wazi na sio jambo la kawaida. “Huyo fedhuli wako bangi zimemparamia! naskia anafukuza watu na mapanga huko nje” akajibu kwa jeuri, “uliskia watu wanazaa na wewe ukazaa! Utakoma this time!” Akazidi kuleta kejeli na kumsazaa mwenziwe “subiri kuitiwa mzoga, maana waja hawatambakisha”.

 

Maneno hayo yalizidi kumkang’anya na kumtia wasiwasi mamake Khamisi hata mwili ukamuisha nguvu na kushindwa kujibu, ila alisimama na kutafakari maneno yale, “hivi kweli anamuongelelea Khamisi ama naye keshapigwa puza”. Maana alimjua mwanawe Khamisi kijana mpole sana hivi leo alfu ulela za kuzunguka na mapanga wapi na wapi na Khamisi. Moja jumlisha moja haikuleta mbili kwake kabisa, aliingia chumbani na kuangalia taswira mle ndani, kile kimya kilichokuwa mle ndani kilikinzana na fikra zake, maana akili yake ilikuwa fikra za ghasi tu. Mboni zake ‘zikaangukia’ kwenye albamu lile, kurasa iliyokuwa wazi ni ya marehemu mumewe. Akasogea na kulichukua albamu lile, akatazama kwa uzuri na makini ile picha utadhani anajaribu kuleta kumbukumbu za kumfahamu aliyekuwa katika picha ile. Wajihi ulikuwa umebadilika teyari! Kiwingu cha majonzi kikampa kivuli, akajifikicha macho na kanga yake aliyokuwa amejitanda mabegani. Akavuta pumzi polepole ya kutuliza kichwa na akafunga albamu lile chap! chap! na kufungua kabati na kutoa kanga nyengine ya kujitanda kichwani, kanda mbili mguuni, akavuta mlango na kutia komeo. Fyuuuup! Na kutoka haraka, kutokomea.

 

Umati ulianza kufurika kwa haraka! Kila mtu aling’ang’ania kupata sehemu nzuri ya kusimama ili kujionea matokeo ya bure. Kweli limbukeni hana siri! kama ibada zingekuwa zinajazwa kwa mtindo huu! wala Mola asingetuletea maafa yeyote na riziki zingekuwa kwa wingi. Wenyewe wanasema uswahilini hakuna dogo, madogo hufanyika uzunguni. Kila anayefika pale alitaka kujua kilichokuwa kinajiri, ila majibu sasa yalitegemea na pahali ulipokuwa umesimamia. Habari zilizotoka kwa ‘wapambe’ waliokuwa mbele ya tukio hazikushahabiana na zile zilizokuwa zikipeperushwa kwa wale waliokuwa nyuma. Kila zilipowafikia waliokuwa nyuma zilikuwa tata zaidi kila mmoja ‘aliongeza chumvi’ kwa kiasi alichokipenda yeye. “Eti naskia kuna jini limeingia mle ndani” mmoja aliropokwa, mwengine akamkata juu kwa juu “sio jini babu ehh! ni joka kubwa limo humo ndani”. Sasa hio ndio ilikuwa hali halisi ya uswahilini, wanahabari wengi walishafutwa kazi kwa kuchukua habari za wanakijiji bila kuzihakikisha mchipuko wake. Mara kidogo kamsa zilisikika “usiniuwe mi toka nikutoke wa mzee wako, mbona watafuta laana mtoto wewe!”. “Kwani nitaanza kuzipata mimi, we bora nikupeleke jongomeo”. Umati ukazidi kupigwa na butwaa! Maana zile habari za awali za majini na nyoka hazikuonekana kuwa na ukweli wowote kutokana na magombano waliyoyaskia.

Fujo ziliendelea mle ndani, kweli mapambano yalikuwa yamechacha  vyombo vilisikika vikianguka. Watu nao nje hamu na hamumu ziliwazidi kila mayoye yalipozidi. Waliamua wasingeweza kukosa uhondo wote huo, maana milango na madirisha yalikuwa yamefungwa yote na hawakupata kuona lolote. Jagina moja likatokea ili ‘kutafuta suluhu’ na kusukuma watu nyuma, akaanza kuonesha madoido kwa kukaza misuli yake ya mikononi. Watu walimshangilia na kumtia mori, akajawa na ushujaa akaja mbio kwa fujo, na kupita na mlango wa nje kwa bega lake. Naye kweli alikuwa na nguvuze, ule mlango kuuvunja kwa kishindo kimoja ni jambo la kupewa kongole kwa kazi nzuri aliyoifanya.  Naye ‘ushujaa’ ule ulikuja na gharama alianguka kwa kishindo ukumbini na kujipiga na meza. Maskini ya Mungu! Alilia kama kitoto kidogo, bega lilikuwa khalas! tayari lilikuwa limevunjika. Watu wakaanza kumiminika kuingia mle ndani, hata hawakudiriki kumpa usaidizi wa kwanza ‘shujaa’ wao aliyewavunjia mlango. Walimuacha akigaragara chini na kumruka bila hata ya kumjali na lolote. Punde si punde kila mtu alionekana akikimbilia kutoka nje. Mlango ukageuka ‘mdogo’ watu waliparamiana na kusukumana ili wapate nafasi ya kuregea walipotokea. Vilio viliskika tu sana kwa wingi,na wale waliokuwa nje walishindwa kwa nini wenzi wao wanaregea tena kwa kishindo. “Anakuja tayari kashamaliza huko ndani”………………….

 

Mwandishi: Mtoto Wa Katama

Mara Khamisi alitulia kwa ghafla baada ya kufungua kurasa nyengine ya albamu lile, akasita kwa muda, macho yakawa mazito na machozi kuanza kumlengalenga. Akawa baridi na ukiwa ukamtawala kwa ghafla, akajiona mnyonge ajaabu na kufunga albamu na baadaye kulifungua tena. Picha iliyofuatia ilikuwa ni ya marehemu babake. Ni miaka kumi imepita tangu kumpoteza babake katika ajali ya barabarani iliyonaswa na vyombo vya habari karibia vyote. Taarifa za kifo cha babake zilimpa mshtuko zaidi nina yake aliyekuwa mtegemezi zaidi, hakujua angeanzia. Baba Khamisi ndiye alikuwa anatarazaki pekee yake. Tena Baba Khamisi shughli zake zilikuwa nadhif kabisa, alisifika kwa kufanya adala baina ya watu na zaidi kwenye shughuli zake za kila siku. Lakini kinaya kilikuwa ni madhila na unyanyasaji mamake Khamisi aliyopitia kutokana na nduguze mumewe. Haya yote Khamisi aliyaelewa kabisaa na alikuwa ameweka nadhiri kitambo ya kupanga kisasi.

Njia mbili za machozi zilibubujika kama mtoto mdogo, kile ambacho hakuelewa zaidi ni watu alowaita ami zake kuwageuka bila hata huruma na kuwaonyesha unyama wa aina ya mwisho, akajiuliza hivi kweli damu ina uzito wowote? Anaikumbuka vizuri ile siku aliposhuka eda mamake kulikuwa na timbwili la aina yake. Ami zake walikuja na kupiga wanawake kisaramgambo waliokuja kumfariji mamake Khamisi,  walijaza nyumba ya kina Khamisi na umati ili kushuhudia tafarani waliyoileta ya kugombea hati miliki za ardhi za marehemu babake. Mama kwa unyonge akaona yote ya nini haya alijionea aepukane na balaa zote na kuwaachia waondoke na stakabadhi hizo muhimu karatasi. Zegere lote hilo likitokea ndio mwanzo kuanza kubaleghe na angejiletea ‘laana’ tu! Bure kwa kuingililia mgogoro ule wa watu wazima, lake likawa ni jicho. Albamu lile lilizidi  kumkumbusha mavi ya kale, kweli hayaachi kunuka! Fikra mpya zikamjia “mimi nishakuwa rijali sasa, na nina haki ya kurithi alichoacha marehemu babangu” alijinong’oneza.

Ari ya kulipiza kisasi ikazidi kumtawala, machozi nayo yakazidi kumdondoka, roho nayo ikafungama na kujisokota na machungu ya miaka yote ile. Mwili nao ukawa unatetema na kusisimka, utasema kapigiwa ngoma za kula nyama mfu za wachawi kilingeni. Akaanza kuguna na kunguruma kama simba, sasa mwili ulizidi kutetemeka utasema zezeta yaani kiufupi mwili mzima ulikuwa chini ya ‘milki’ mpya, mara ghafla akaanza kupiga nduru “ Uwiiii Leo nauwa babu, natamani harufu ya damu sana” akapayuka payuka huku mate yakimdondoka. Yallahu yalamu, mizimu ya kwao ilikuwa ishaenuka, nani atakayemrudisha chini? Wenyewe husema yakwao yakienuka hata kwa lifti hayashuki. Aliinama na kuchochomeza mkono katika mojawapo ya tendegu la kitanda, baada ya kupapasa alichomoa sime Enhe! Kwa kweli kilikuwa kimeumana aisee! Pyuu! Aliponyoka tu utadhani panya aliyejinasua katika mtego baada ya mrefu wa kukata tamaa na maisha , hata mlango aliuacha wazi ng’waa wote alisahau mle ndani kulikuwa na ‘uhai’ wao wote, japo vitu vilivyokuwa ndani havikuwa na thamani sana lakini ndivyo vilivyowatunza na urathi waliobaki nao pekee. Haswa haswa dhahabu za mamake mara nyingi alishayeyusha vipande kwa sonara ili kukidhi mahitaji ya nyumbani. Mara nyingi aliepuka mialiko ya harusi za uswahilini kwa kukosa herini na bangili, aliogopa kuwa ‘topiki’ ya mtaani, sababu ya kuyeyusha vito vyake ni, wakati mwengine huja kipindi ikawa hana chochote kabsaa sasa na inambidi akate pua ili aunge wajihi. Wajihi ambao ni akina Khamisi na ndunguze, wajihi ambao Khamisi alikuwa anaenda kuuharibu licha ya matatizo aliyopitia mamake mzazi.

“ Uwiiii! Jamani huyo chungeni ana silaha. Atamwaga damu” kamsa zilisikika kutoka kila sehemu, kila mtu alikimbia njia yake kuokoa roho yake,barabara ikaleta taswira ya Rwanda watutsi wakiwakimbia wahutu, wazungu wenyewe wangesema ‘running for your dear life’. Wale waliokuwa barabarani wakiuza bidhaa zao waliziacha na kutokomea wasijulikane wanakokimbilia ililkuwa ni tafarani moja kwa mbili, wengine walijikung’waa na kuanguka, mmoja alijipata akiogelea katika sufuria la uji wa ngano moto, Lo! Alishaharibia watu kiburudisho chao cha muda wa baada ya alasiri bora hata angeangukia kwengine na kujifia. Hivi watu wote wakapati wapi sharubati ya kushukishia viazi vya karai. Ila mchezo kando yale matukio yaliyokuwa yakiendelea pale yalikuwa ni ya mguu niponye, utasema kila mtu anakimbilia hukumu yake ya siku ya kiyama baada ya parapanda kupigwa na malaika Israfil . Mara Khamisi akapita mbio katika barabara ile na kushika uchochoro mwengine, jambo hilo lilimtia wasiwasi zaidi huyo aliyemtangulia katika kichochoro hiko, kosa lake kubwa kuaachana na wenzake na kuamua kukimbia peke yake na wenziwe kuchukua njia nyengine. Sasa hapo ndio muda wa kujilaani na kujijutua kuachana na wenzio maana waswahili husema kifo cha wengi ni harusi, hivi yahkhe leo anajiona akitolewa roho pekee yake. “Kesha pagawa! Wallahi ameshakuwa chizi, lakini ole wake akili zikimarudia atatulipa biashara zetu sote” nyuma sauti ziliskika zikilaani kwa hasira. Lakini Khamisi hakuwa na shida nao, ni umbea wao tu uliowachongea, yaani hivi ukiona mtu akija mbio na panga na nyinyi eti mnaamua kukimbia….eti ehh?  Swali hilo. Yaani mnakurupuka tu ovyoo! Na kujijeruhi na kusababisha hasara biashara zenu…kwani hamjawahi kuona wamasaai wakizunguka na sime zao viunoni? Na wala hamjawahi kukimbia, hivi leo mnamuonea ajabu Khamisi. Khamisi naye yeye alikuwa anakimbizwa na ajenda zake, mbio zote hizo alikuwa akieleke akwa ami zake…………………