Mwandishi: Naima Baghozi

Unaweza kusoma sehemu ya kwanza ya hekaya hii: https://lubnah.me.ke/kinyonga-na-tausi-sehemu-ya-1/

 

“HAHAHA HAHAHA HEHEHE….” Aliangua kicheko kile huku akiwa chali mara akijipindua hivi na vile maana aliona ajabu kuwa Kinyonga aliamini ataweza kujigeuza rangi ya mwili wake.

Kinyonga alipoona namna anavyocheka paka kwa stihizai alikasirika na kuondoka huku akilini akijiambia, “Nitamwonesha huyu Paka kuwa naweza kujigeuza!”

Basi akaendelea na safari yake mpaka akatokezea pahala penye miti kiasi na hapo akamuona Tumbiri akirukaruka kutoka mti mmoja hadi mwingine katika hali ya kucheza cheza . Alipomuona Kinyonga akasita katika michezo yake.

“Kinyonga, habari ya siku nyingi? Kitambo sijakuona, ulikuwa wapi?” Akajibu Kinyonga : “Nilikuwa huko mbali kwenye boma la Tausi.” Tumbiri akamuuliza : “Ulikuwa unafanya nini muda wote huo?” Nae akamjibu: “Nilikuwa nikiushangilia na kuufwatilia uzuri wa rangi zake na hasa anapochanua mkia wake. Zile rangi zake zinanipendezea sana mpaka nimetamani kuwa nazo. Je, unaweza kunishauri vipi nitaweza kuzipata rangi hizo nzuri mwilini mwangu?”

Tumbiri akamtazama Kinyonga bila kumwambia kitu kwanza kisha akamwabia: “Hmm! Subiri nifikiri kidogo .” Wakaketi kimya kidogo huku Tumbiri akijikuna kichwa akiwa mwenye bahari ya mawazo. Mara akaruka ghafla juu na chini akimwambia Kinyonga kuwa ameshapata jawabu la suala lake. Kinyonga nae akainua uso wake kwa bashasha na furaha nyingi akimtaka Tumbiri amjibu kwa haraka. “Niambie rafiki yangu, wewe ndiye rafiki yangu wa kikweli kweli.” Tumbiri akamnyamazisha kwa kumwambia: “Unaona giza limeanza kuingia , bora tulale, tupumzike hadi asubuhi. Maoni yangu ni kuwa tukusanye maua ya kila rangi kama mekundu , manjano, zambarau, kijani na kadhalika. Kisha tuyatie maji kidogo na kuyaponda ponda mpaka yatoe rangi, hiyo rangi ukijipaka mwilini mwako kila sehemu rangi tofauti utakuwa mrembo kama Tausi. Unaionaje fikra yangu?”

Kinyonga alishindwa kuficha furaha yake na akajibu kwa wingi wa bashasha: “Maoni yako ni mazuri sana na naona ni njia nzuri kabisa. Haya tulale basi ili tuweze kurauka.”

Basi kila mmoja akashika upande wake na kulala lakini Kinyonga kwa ile hamu aliyokuwa hakuweza kulala vizuri maana aliona hata asubuhi haitofika…

Hata kabla ya kupambazuka vizuri alikuwa tayari kuianza hiyo shughuli ya kutafuta maua . Kwa vishindo vyake na kufurukuta kwake Tumbiri akainuka nae kwa kughasika akamuuliza Kinyonga : “Mbona unafanya vishindo mpaka umenikatiza usingizi wangu? Mwenyewe nilkuwa ninaota ndoto nzuri …”

“Ndoto gani ya saa hizi? Huoni asubuhi imeshafika? Inuka tukatafute hayo maua.” Tumbiri akajibu: “Wewe hata umelala? Sasa hata mwangaza haujatoka. Sasa tutaona nini hivi? Tusubiri kidogo zaidi.” Basi Kinyonga akawa hana budi ila kusubiri mwangaza utokeze vizuri maana alijua bila ya usaidizi wa Tumbiri hatoweza kufanya lolote.

Akawa anaenda mbele akirudi nyuma huku akijipatia vidudu akijilia. Mwangaza ulipojitokeza vizuri Tumbiri akamwambia:”Haya rafiki yangu wakati umewadia. Twende tukakusanye maua tuje tuanze kazi.”

Kinyonga hakuweza kuficha hamu yake akasema: “Haya twende zetu.” Wakaondoka na kabla ya kufika mbali wakakiona kiwanja kilichopambika kwa maua ya rangi ainati, yaani kila rangi waliotaka waliipata hapo. Nao hawakuchelewa kuanza kukusanya. Kinyonga alikuwa amebahatika kwani Tumbiri alikuwa na mikon kama ya binadamu kwa hivyo kazi ilifanyika vizuri. Muda si muda Tumbiri akasema: “ninaona haya tuliyoyakusanya yanatosha. Twende zetu.”

Wakarudi maskani yao. Tumbiri akachukua maji kidogo na jiwe na kuanza kuyaponda ponda yale maua kila rangi kivyake. Yalipotoa rangi alimwambia Kinyonga “Haya rafiki yangu rangi zote ziko tayari njoo nikupake upate kurembeka.”

Kinyonga akasogea mpaka alipo Tumbiri naye akaanza kumpaka rangi moja baada ya nyingine yaani kijani kisha nyekundu kisha zambarau kisha manjano na rangi nyinginezo kwa ustadi kabisa. Alipomaliza akamwambia : “Eeh Kinyonga umependeza kweli. Sasa sogea ukae penye jua upate kukauka vizuri. Kinyonga akaenda palipo na jua huku akiuliza : “Nimependeza kweli?” Tumbiri akamjibu kuwa kila atakayemwona angemwonea wivu.

Basi akajituliza juani na kwa sababu usiku hakulala vizuri akapatwa na usingizi. Ni kama alikuwa akiota jua.Aliposhtuka ilikuwa imeshafika adhuhuri. Akamuaga Tumbiri kuwa anaaondoka: “Mimi sasa ninarudi nikamwonyeshe paka aliyekuwa akinicheka na kombamwiko aliyesema sitoweza geuka na hasa huyo tausi aliyenidharau.”

Tumbiri akajaribu kunasihi abaki nae zaidi kidogo lakini alikataa kata kata . “Samahani rafiki yangu lakini hujui ile hamu niliyo nayo kuwafikia hao walionidharau. Tutaonana siku nyingine na asante sana kwa usaidizi wako rafiki yangu, wewe peke yako ndiye uliyesimama na mimi.Haya kwaheri ya kuonana…”

“Kwaheri ya kuonana.” Tumbiri akamjibu.

Kinyonga akaanza safari yake ya kurudi maskani yake anapoishi na Tausi. Akatembea kwa muda mrefu, mara akamwona Paka ,akamwita: “Paka, Paka wajidai hunioni. Niangalie, niangalie uone urembo wangu.”  Huku akijigeuza hivi na vile ili aone rangi zake tofauti tofauti. Akaendelea: “Mbona sasa hunicheki, nicheke kama ulivyonicheka mwanzo. Hahahaha-hehehehe.” Akimuigiza vile alivyomcheka mara ya kwanza. Paka akamjibu kwa mshangao: “Aah! Kinyonga, huyu ni wewe kweli?” huku akimzunguka zunguka. Kinyonga hakumjibu kitu. Aliondoka tu na kwenda zake akimwacha Paka kinywa wazi.

Basi safari ikaendelea njia nzima maringo yakimzidi na pia akitafakari vile alivyomuacha Paka na mshangao. Kinyonga akaendelea mpaka alipokutana na kombamwiko. Naye pia hakusita  kuona maajabu ya mabadilko ya Kinyonga ,akamuuliza: “Kinyonga, ni wewe au ni macho yangu? Umekuwa mrembo kweli. Umefanya nini hadi kupata rangi hizo nzuri nzuri mwilini mwako?”

Kinyonga akamjibu: “Sikukosa wa kunisaidia, ingawaje nyinyi huku mlikataa kabisa.”

“Sio tulikataa nawe, ni kuwa hatukujua tukusaidie vipi. Niambie basi ulimpata nani wa kukusaidia?” Kwa maringo zaidi kinyonga akaanza kumwelezea namna Tumbiri alivyomsaidia tangu mwanzo hadi mwisho. Alipomaliza akawa anamuaga Kombamwiko hamu yake kubwa ni kumfikia Tausi ili auone urembo wake. Mara kwa ghafla kukateremka mvua , mvua iliyokua haitarajiwi. Kombamwiko mbio mbio akaingia kwenye kipango chake ili kujikinga na mvua na Kinyonga maskini akawa anahangaika hajui ajifiche wapi, mwisho akapata majani ya mkungu yaliokuwa yameanguka chini akajibarizi hapo.

Haikuchukuwa muda mrefu, mvua kama ilivyoshuka kwa ghafla na pia ikasimama kwa ghafla na pia ikasimama kwa ghafla. Kukawa kimya kwa muda mfupi.

Kombamwiko akatoka makaoni pake na kuangalia Kinyonga alikokuwepo huku akimuita, : “ Kinyonga, Kinyonga..,uko wapi?”

Kwa utaratibu Kinyonga akajitokeza na kujibu “ Mimi niko hapa..” Akanyamaza ghafla kwa kumuona jinsi Kombamwiko alivyokuwa akimtizama kwa sura ya huzuni kubwa.

“Mbona unaniangalia hivyo?” Akauliza. Jawabu alilopata ni: “Urembo umeshakutoka rafiki yangu …”

“Ukimaanisha nini?” Kinyonga akashangaa. Kombamwiko akauliza: “Umesahau kuwa si maumbile yako bali ni rangi tu ulizojipaka?”

“Kwa hivyo…?” Kinyonga akarudi kuuliza. “Kwa hivyo ile mvua iliyokupiga imebakisha michirizi ya rangi tu mwilini mwako tena zimechanganyika changanyika. Hebu tizama chini yako huoni mitiririko ya rangi?”Maskini Kinyonga akajitizama na kuona michirizi ya rangi iliyokuwa ikitiririka kutoka mwilini mwake. Moyo ulimuuma na machozi kumbubujika buji buji akiuona urembo wake huoooo unamtoka.


Itaendelea karibuni…

 

Write A Comment